Pages

Wednesday, 1 June 2022

UFAHAMU: UKOSEFU WA MVUA

Nchi zetu za Afrika zinakumbwa sana na ukosefu wa mvua. Inasemekana ya kwamba jangwa linazidi kutanda katika bara hili, kwa hivyo ni wajibu wetu kujiandaa na kuchukua hatua kadha wa kadha ili tuweze kupambana na ukavu huu, kwani wahenga walisema, “Uwahi udongo uli maji.”

Kwa hakika ukavu huu unasambaa katika bara hili na unatutia hofu kubwa. Imekuwa sana tunategemea nchi za kigeni kutusaidia. Tukichunguza zaidi sababu kubwa ya ukosefu wa mvua ya kutosha ni ukataji wa miti. Kwa hivyo tuhakikishe kuwa tutapanda miti kwa wingi wakati wa mvua. Serikali ya Kenya inahimiza sana upandaji wa miti katika sehemu mbalimbali za nchi. Pia lazima tuhakikishe kwamba baada ya mche kupandwa, kufanywe mipango na kupatikane watu ambao wataiangalia na kuipalilia hadi itakapokuwa mkubwa. Ni wazi kwamba tumetilia mkazo wa kupanda miche lakini hatujazingatia miche hii kuangaliwa kwa kunyunyiziwa maji wakati wa ukame.

Hatua ya kuchimba visima, katika sehemu zenye ukavu ni jambo la muhimu sana, kwani maji ya visima yataweza kutumika majumbani na pia kunyunyizia mimea. Maji kwa binadamu ni kitu muhimu sana kwa sababu bila ya maji hakuna uhai. Huko Australia, visima vingi vimechimbwa katika sehemu zenye ukame kwa minajili ya kuwapatia wakazi wa sehemu hizo maji ya nyumbani, mifugo na kunyunyizia mimea.

Maji ya mvua na yale yanayochuruzika mitaroni, hukusanywa na kutumiwa kwa kunyunyizia mimea. Mashamba yanayonyunyuziwa maji ya aina hii, hunawiri na kustawi sana. Maji ya mito ambayo huchuruzika baharini, lazima tuyatumie baada ya kuiondoa chumvi ndani yake. Vile dana, tujaribu tuwezavyo kupanda mimea ambayo itatupa chakula cha kutosha ili tuweze kujitegemea badala ya kuzitegemea nchi za kigeni.

 

 

(a) Mwandishi ametumia methali “uwahi udongo uli maji” akimaanisha nini hasa?

(b) “Haitoshi tu kupanda miche na kutulia”. Kulingana na yaliyomo katika taarifa hii, ni hatua gani zingine zinazohitajika ili kufaulu katika mradi huo wa upanzi?

(c) Taja jitihada zozote mbili zinazochukuliwa na serikali ili kukabiliana na shida ya ukosefu wa mvua / maji.

(d) Kwa nini maji ya baharini hayatumiwi moja kwa moja?

(e) Kwa nini nchi nyingi za bara la Afrika zinategemea nchi za kigeni?

(f) Maneno yafuatayo yametumiwa kuleta maana gani?

(i) Kutanda____________________________

(ii) Miche_____________________________

(iii) Kunyunyizia________________________

(iv) Hunawiri__________________________

(v) Kustawi___________________________

No comments:

Post a Comment

Please leave your comment/question or suggestion.